Home » » WAZIRI KOMBO AMWAKILISHA RAIS SAMIA KWENYE UAPISHO WA RAIS WA IRAN

WAZIRI KOMBO AMWAKILISHA RAIS SAMIA KWENYE UAPISHO WA RAIS WA IRAN

Written By CCMdijitali on Friday, August 2, 2024 | August 02, 2024



Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo na Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Mhe. Masoud Pezeshkian wakiwa katika mazungumzo yaliyofanyika katika Ikulu ya nchi hiyo jijini Tehran


·      Afanya mazungumzo na Rais huyo

·      Mikakati ya kukukuza zaidi uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi yawekwa

 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo alimwakilisha wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwenye sherehe za uapisho wa 14 wa Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Mhe. Masoud Pezeshkian iliyofanyika katika viwanja vya Bunge vya Nchi hiyo jijini Tehran, tarehe 30 Julai, 2024.

 

Waziri Kombo aliwasili nchini humo alfajiri ya tarehe 30 Julai 2024 ambapo baada ya kushiriki katika sherehe hizo za uapisho aliendelea kujumuika na maelfu ya Wanadiplomasia na Viongozi wa Nchi na Serikali kutoka sehemu mbalimbali duniani kushiriki katika dhifa iliyofanyika katika Ikulu jijini Tehran. 

 

Waziri Kombo, alimpongeza Mhe. Pezeshkian kwa ushindi wake katika uchaguzi  wa Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran uliofanyika hivi karibuni, na kuongeza kusema kuwa Iran na Tanzania zina uhusiano wa karibu wa kiutamaduni na kihistoria ambao ulianza miaka mingi iliyopita wakati kundi la Wairani kutoka Mji wa Shiraz lilipohamia Zanzibar na kueneza utamaduni wa Iran na lugha ya Kiajemi.

 

Mbali na kushiriki katika sherehe za uapisho huo, Waziri Kombo alifanya mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Mhe. Masoud Pezeshkian yaliyofanyika Ikulu jijini Tehran tarehe 31 Julai, 2024, akiwa ni Waziri wa Mambo ya Nje wa kwanza na pekee aliyepata fursa ya kuzungumza na Rais huyo muda mfupi baada ya kuapishwa kwake.

 

Mazungumzo hayo yalijikita kujadili kuhusu masuala mbalimbali ya kudumisha na kukuza zaidi ushirikiano katika nyanja mbalimbali ikiwemo siasa, kijamii, utamaduni na uchumi kati ya nchi hizo mbili. 

 

Kwa upande wake Rais wa Iran Mhe. Pezeshkian katika mazungumzo yaliyofanyika kwa takriban dakika 25 huku pande zote mbili zikionesha furaha, shauku na umakini, alielezea furaha yake na kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutuma ujumbe uliowasilisha salam za pongezi na kushikiri katika sherehe za uapisho wake.  

 

Mhe. Pezeshkian aliendelea kueleza kuwa Tanzania na Iran kwa muda mrefu zimekuwa zikishirikiana katika nyanja mbalimbali, hivyo katika kipindi cha uongozi wake atahakikisha uhusiano huo unaedelea kukua zaidi na maeneo mengine mapya ya ushirikiano yanafunguliwa kwa maslahi ya pande zote mbili.

 

“Kwa muda mrefu tumekuwa na ushikiano mzuri kati yetu katika maeneo mbalimbali, nitoe raia kuwa sasa niwakati muafaka ufanyike mkutano wa mashauriano wa tume ya uchumi ili iandae rasimu ya Hati za Makubaliano ya Ushirikiano ya pande zote mbili” alisema Rais Mhe. Pezeshkian

 

Kwa upande wake Waziri Kombo alieleza baadhi ya mikakati na hatua mbalimbali zinazoendelea kutekelezwa na Tanzania katika kudumisha na kukuza zaidi ushirikiano na Iran ikiwemo mandalizi ya kufanyika kwa mkutano wa Tume ya Pamoja ya Ushirikiano (JPC), Kongamano la biashara kati ya Tanzania na Iran, kubadilishana ziara za viongozi kufanya mapitio ya suala la Visa rejea (referral visa). 

 

Vilivile, Waziri Kombo alifanya mazungumzo na Kaimu Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Mhe. Ali Bagheri ambapo walijadili na kukubaliana utekelezaji masuala mbalimbali muhimu katika kukuza ushirikiano wa kidiplomasia na kiuchumi.



Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Mhe. Masoud Pezeshkian walipokutana kwa mazungumzo katika Ikulu ya nchi hiyo jijini Tehran, tarehe 30 Julai, 2024, alipokwenda kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan katika sherehe za kuapishwa kwa Rais mpya wa Iran.


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo akiagana na Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Mhe. Masoud Pezeshkian mara baada ya hafla ya chakula cha usiku kilichoandaliwa na Rais wa Iran kwa ajili ya wageni wake.

Share this article :
 
Support : #BegaKwaBegaNaMamaSamia | JAK | CCM Arusha
Copyright © 2011. CCM Dijitali - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Jasper K
Proudly powered by Blogger
Link