NAIBU WAZIRI PINDA AELEKEZA UENDELEZAJI MIJI KUZINGATIA MIPANGO KABAMBE

Na Munir Shemweta, WANMM Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Geofrey Pinda amezielekeza Halmashauri zote nchini kuhakik...

Latest Post

Wasomi, wanasiasa wachambua 2017

Written By CCMdijitali on Friday, December 29, 2017 | December 29, 2017

Makamu Mkuu mstaafu wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agustino (SAUT), Dk Charles Kitima

 Imeandikwa na Matern Kayera - Habari Leo

WASOMI na Wanasiasa maarufu nchini wamesema kuwa wanaridhishwa na hali ya kisiasa iliyopo nchini kwa kipindi chote cha mwaka 2017.

Kuridhishwa huko kumetokana na hali ya utulivu na utendaji makini wa Serikali ya Awamu ya Tano ambayo inajali watu wake. Makamu Mkuu mstaafu wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agustino (SAUT), Dk Charles Kitima aliliambia gazeti hili jana kuwa wananchi wameridhika kutokana na utendaji wa serikali.

Alisema serikali iliyopo madarakani imejali kwa kiasi kikubwa maisha ya watu wake hasa katika suala la usalama. Dk Kitima alisema pamoja na changamoto za kiusalama zilizotokea kwenye baadhi ya maeneo nchini kama vile Kibiti mkoani Pwani, hali ya usalama nchini bado nzuri.

“Watu wanafuata sheria, lakini pia utendaji wa watumishi wa umma nao umebadilika na umekuwa mzuri, kwa kipindi hiki tumeona wananchi wakihudumiwa vizuri kwenye taasisi za umma,” alieleza Dk Kitima. Hoja hiyo ya kuwepo kwa mabadiliko chanya ya kisiasa nchini imeungwa mkono na Mbunge wa Mbinga Mjini kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Sixtus Mapunda.

Mapunda alisema kuwa hali ya kisiasa inazungumzwa katika maeneo matatu, yaani kiuchumi, kijamii na kisiasa. Alisema kwa kipindi cha mwaka 2017, hali ya kisiasa katika uchumi imekuwa nzuri na tulivu kutokana na kuwepo kwa uhakika wa chakula nchini. Alisema taifa lina chakula cha kutosha na kinapatikana kwa urahisi hali inayoleta utulivu. Kwa mujibu wa Mapunda, uwepo wa chakula cha kutosha unadhihirishwa na kuwepo kwa ziada ya chakula hasa mahindi katika mikoa na wilaya mbalimbali nchini ikiwemo Wilaya ya Mbinga.

Mbali na utoshelevu wa chakula unaoleta utulivu, Mapunda amesema katika nyanja ya uchumi pia kumekuwa na ujenzi wa miradi mikubwa ya maendeleo pamoja na manunuzi ya ndege mpya.
Akitolea mfano kuanza kwa ujenzi wa reli ya kisasa kutoka Dar es Salaam kwenda Mwanza na baadaye Kigoma, pamoja na ununuzi wa ndege mpya, Mapunda alisema mambo hayo ni muhimu siyo tu kiuchumi lakini pia katika kuleta utulivu wa kisiasa. Alisema kutokana na Serikali kununua ndege mpya, wananchi wengi wanamudu kusafiri kutokana na kushuka kwa bei.

Alisema haikuwa rahisi zamani kwa watu wengi kusafiri kwa ndege kutoka Dar es Salaam hadi Songea kwa kuwa nauli yake ilikuwa Sh milioni 1.2 tofauti na sasa ambapo nauli ni kati ya Sh 280,000 na 360,000. “Kisiasa, serikali imefanikiwa kuweka utulivu nchini; watu wanafuata utawala wa sheria na hakuna aliye juu ya sheria, watu wa chini ambao hawakuwa na sauti kwa muda mrefu, hivi sasa wanajisikia kuwa nchi hii ni ya kwao,”alieleza Mapunda.

Kwa upande wake, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Benson Bana alisema kisiasa, taifa limefanikiwa kulinda na kuheshimu tunu muhimu kama vile amani, umoja na Muungano na kuweka kando migawanyiko kwa misingi ya kikanda na migogoro kama vile ya wafugaji na wakulima. Kwa mujibu wa Dk Bana, kisiasa pia kumefanyika maamuzi magumu na mazuri kwa mambo muhimu ya kitaifa.

Aliyataja baadhi ya maamuzi hayo kuwa ni pamoja na kudhibiti vitendo vya rushwa, ufisadi na uhujumu uchumi pamoja na vigogo mbalimbali kufikishwa mahakamani. Mambo mengine ni msamaha wa kihistoria wa wafungwa uliofanywa na Rais Magufuli. Alisema kitendo cha Rais kutoa msamaha kwa wafungwa waliohukumiwa kunyongwa na wengine kifungo cha maisha, kimeleta upenda na furaha kwa wananchi.

Changamoto Pamoja na mafanikio hayo kisiasa na kiuchumi, bado zipo changamoto kadhaa zilizoelezwa kuhitaji kufanyiwa kazi likiwemo suala la katiba mpya, fursa za wanasiasa kufanya shughuli zao pamoja na ajira kwa vijana.

Akizungumzia baadhi ya changamoto hizo, Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Profesa Mwesiga Baregu alisema kuwa hali ya kisiasa nchini kwa mwaka 2017 haikuwa nzuri kutokana na kukamatwa kwa baadhi ya watu wakiwemo wanasiasa na kisha kuachiliwa bila maelezo.

Alisema ili kujenga demokrasia ya vyama vingi na yenye ushindani, inatakiwa suala la mchakato wa kupata katiba mpya uendelee hadi mwisho kwa kipindi cha mwaka 2018. Alisema mambo kama vile vita dhidi ya ufisadi na rushwa yatafanikiwa kama yatawekwa kwenye katiba.

Kwa upande wake, Dk Kitima alisema kuwa mahusiano ya vyama vya siasa kwa mwaka 2017 hayakuwa mazuri. Alisema ni vyema vyama vya siasa kujenga tabia ya kuwa na majadiliano kwa mambo muhimu ya kitaifa kama vile uchumi wa viwanda. Kuhusua tatizo la ajira kwa vijana, Dk Kitima alisema linasababishwa na ukosefu wa shughuli za kiuchumi ambazo zingewaunganisha na masoko ya nje.

Tanzania nchi yangu.

Tanzania nchi yangu.

KILIO CHA WADAU WA SEKTA YA UWINDAJI WA KITALII NCHINI CHASIKIKA SERIKALINI

 Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akizungumza na wadau wa sekta ya uwindaji wa kitalii katika mkutano uliondaliwa na Wizara yake mjini Dodoma jana kwa ajili ya kujadili mikakati mbalimbali ya kuimarisha sekta hiyo ikiwemo utekelezaji wa azma ya Serikali ya kuanzisha utaratibu mpya wa utoaji wa leseni za vitalu vya uwindaji wa kitalii kwa njia ya mnada. Kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Mej. Jen. Gaudence Milanzi na Naibu Katibu Mkuu, Dk. Aloyce Nzuki (kulia).

 Mwenyekiti wa Chama cha Wamiliki wa Kampuni za Uwindaji wa Kitalii nchini, Michael Mantheakis (kulia) akiwasilisha mapendekezo yake katika mkutano wa wadau wa sekta ya uwindaji wa kitalii katika mkutano uliondaliwa na Wizara ya Maliasili na Utalii mjini Dodoma jana kwa ajili ya kujadili mikakati mbalimbali ya kuimarisha sekta hiyo ikiwemo utekelezaji wa azma ya Serikali ya kuanzisha utaratibu mpya wa utoaji wa leseni za vitalu vya uwindaji wa kitalii kwa njia ya mnada.

 Baadhi ya wadau wa sekta ya uwindaji wa kitalii wakiwa katika mkutano huo.

Baadhi ya watendaji wa Wizara ya Maliasili na Utalii na Taasisi zake wakiwa katika mkutano huo.

Na Hamza Temba, Dodoma
...............................................................
Serikali imesikia kilio cha wadau wa sekta ya uwindaji wa kitalii nchini na kuamua kuongeza muda wa miaka miwili ya umiliki wa leseni za vitalu 95 vya uwindaji wa kitalii ambazo zilikuwa ziishe muda wake tarehe 31 Desemba mwaka huu (2017).

Uamuzi huo umefikiwa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla wakati wa kikao cha majumuisho na watendaji wa Wizara hiyo muda mfupi baada ya kumalizika kwa mkuano wa wadau wa sekta hiyo ulioandaliwa na Wizara hiyo mjini Dodoma jana.


Akizungumzia uamuzi huo Dk. Kigwangalla alisema, lengo ni kuwapa muda wawekezaji hao ili waweze kujiandaa na mabadiliko ya mfumo mpya wa utowaji wa leseni za vitalu vya uwindaji wa kitalii kwa njia ya mnada ikiwemo kurudisha baadhi ya gharama za uwekezaji walizoweka katika vitalu hivyo.


Awali akizungumza katika mkutano huo wa wadau Mwenyekiti wa Chama cha Wamiliki wa Kampuni za Uwindaji wa Kitalii nchini, Michael Mantheakis alimuomba Waziri Kigwangalla kuwaongezea muda wa umiliki wa leseni zao kuanzia miaka mitano au mitatu na nusu ili waweze kurudisha gharama za uwekezaji walizowekeza katika vitalu hivyo ikiwemo ujenzi wa miundombinu, makambi na vifaa vyake pamoja na maji.


Hata hivyo, Waziri Kigwangalla aliweka wazi msimamo wa Serikali wa kutimiza azma yake ya kuingia kwenye utaratibu mpya wa utoaji wa leseni za vitalu vya uwindaji wa kitalii kwa njia ya mnada na kusema kuwa kamwe haitorudi nyuma na kwamba utekelezaji wa zoezi hilo hauwezi kusubiri muda mrefu kiasi hicho.


Akizungumzia kuhusu hatua ya utekelezaji wa utaratibu huo, Waziri Kigwangalla alisema kwa sasa taratibu za kuandaa Sheria za usimamizi zinaendelea na zinatarajiwa kukamilika mwezi Februari 2018 pamoja na kanuni zake zinazotarajiwa kukamilika mwezi Aprili 2018.


Aidha, alisema mfumo maalumu wa kielektroniki unaandaliwa ambapo maombi yote ya leseni za umiliki wa vitalu vya uwindaji kwa njia ya mnada yatafanyika kwa uwazi kwa njia ya mtandao.


Alisema baada ya kukamilika kwa taratibu zote na mfumo huo mpya wa utoaji wa leseni za vitalu vya uwindaji wa kitalii kwa njia ya mnada na maombi kuwasilishwa, mnada wa kwanza utaanza tarehe 1 Julai, 2018 kwa kuanza kunadi vitalu 61 ambavyo kwa sasa havina wawekezaji.


Mnada wa pili utafanyika mwaka 2020 baada ya kuisha kwa muda huo wa nyongeza wa miaka miwili ukihusisha vitalu 95 vilivyoongezewa muda wa umiliki wa leseni pamoja na vitalu vingine endapo vitabaki katika mnada huo wa kwanza kwa sababu mbalimbali.


Alisema sheria na kanuni zinazoandaliwa hivi sasa zitazingatia mambo muhimu ikiwemo kuwapa nafasi watanzania wenye mitaji midogo kuweza kuingia kwenye biashara hiyo pamoja na kuweka adhabu kali dhidi ya wafanyabiashara watakaohujumu biashara hiyo kwa makusudi.


Mkutano huo wa siku moja ulihudhuriwa pia na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Meja Jenerali Gaudence Milanzi, Naibu Katibu Mkuu, Dk. Aloyce Nzuki, wakurugenzi, wakuu wa vitengo na wakuu wa taasisi zilizopo chini ya wizara hiyo na waandhishi wa habari.


Oktoba 22 mwaka huu (2017) wakati akiongoza kikao cha wadau wa sekta ya Maliasili na Utalii mjini Dodoma, Waziri Kigwangalla alitangaza kufuta leseni za vitalu vya uwindaji wa kitalii zilizokuwa zianze mwezi Januari, 2018 ili kupisha utarartibu mpya wa utoaji wa leseni hizo kwa njia ya mnada ikiwa ni mkakati wa Serikali wa kuimarisha sekta hiyo.


WAZIRI JAFO AVITAKA VITUO VYOTE VYA AFYA KUTENGENEZA BUSTANI ZA KUPUMZIKIA

 Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais,TAMISEMI Mhe. Selemani Jafo(katikati) akikagua ujenzi wa miundombinu ya Afya katika Kituo cha Afya Makole kilichopo katika Manispaa ya Dodoma.

 Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais,TAMISEMI Mhe. Selemani Jafo(Kushoto) akimsikiliza Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Makole kuhusiana na maendeleo ya ujenzi wa kituo cha Afya.

 Jengo la Wodi ya Kinamama kama linavyoonekana likiwa linefikia katika hatua ya Lenta.

 Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais,TAMISEMI Mhe. Selemani Jafo(kulia) akizungumza na Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi(katikati) baada ya ukaguzi wa ujenzi wa miundombinu ya Afya Katika Kituo cha Afya Makole.

Jengo la Chumba cha Upasuaji kama linavyoonekana likiwa katika hatua ya Lenta.
 
Nteghenjwa Hosseah, TAMISEMI.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo amevitaka vituo vyote vya Afya Nchini sambamba na hospital za Wilaya kutengeneza bustani ya kupumzikia kwa wagonjwa wanaosubiria matibabu katika maeneo hayo.

Waziri jafo ameyasema hayo wakati akikagua Ujenzi wa miundombinu ya Afya katika Kituo cha Afya Makole kilichopo Manispaa ya Dodoma na kuutaka uongozi wa Kituo hicho kutenegenza bustani ya kisasa pamoja na kupanda miti ya kutosha ili kutunza matunzingira lakini kupendezesha eneo la hospital.


“Hili Agizo liende kwa Vituo vyote Nchini pamoja na Hospital za Wilaya zilizoko chini ya TAMISEMI kuhakikisha wanaekeleza maelekezo haya katika ameneo yote nataka hospital iwe sehemu ya kupa faraja mgonjwa kwa kupata huduma nzuri lakini pia kusubiria huduma hiyo katika maeneo yanayovutia wakati wote” Alisema Waziri Jafo.

Akikagua majengo matano yanayojengwa katika Kituo hicho cha Afya na kusimamiwa na TAMISEMI Waziri Jafo amesema ameridhishwa na Ujenzi wa miundombinu hiyo ya Afya katika Hospital ya Makole kwani umefuata ramani zilizotolewa na Wizara, unajengwa kwa ubora na uko ndani ya muda wa Utekelezaji. 


“Hivi ndio ninavyotaka wataalamu wangu kujiongeza katika baadhi ya maeneo mfano hapa Mmejenga Mabara kubwa kulingana na wingi wa wagonjwa mnaowahudumia kwa siku sasa sio kwa sababu ramani imeonyesha maabara ndogo basi kila mtu anafuata hivyo hivyo ni lazima tujiongeze kulingana na mahitaji ya ameneo yetu ya huduma” Alisema Waziri Jafo.


Akizungumzia maendeleo ya mradi Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Makole amesema Ujenzi huu umesema ujenzi wa Maabara, chumba cha Upasuaji, Wodi ya Kina Mama, Nyumba ya Mganga pamoja na Ukarabati wa Kichomea Taka utakamilika mapema mwezi February 2017 na Fedha zilizopokelewa kwa ajili ya ujenzi huo zitatosha na kukamilisha ujenzi wa miundombinu yote.


Kituo cha Afya Makole ni miongoni mwa vituo 211 Nchini vilivyopokea/vitakavyopokea Fedha kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya Afya lengo ikiwa ni kuboresha Miundombinu ya Afya ili kuweza kutoa huduma bora kwa watanzania. 


TAMISEMI YA WANANCHI.


UVCCM Taifa wafanya dua katika kaburi la Marehemu Mzee Abeid Aman Karume .

 MWENYEKITI wa UVCCM Taifa Kheir James(kushoto wa kwanza) akitoa Shukrani kwa mapokezi aliyopewa na Uongozi wa Chama cha Mapinduzi Zanzibar chini ya usimamizi wa Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdalla Juma Saasalla (Mabodi) pamoja na SMZ kupitia Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Ayoub Mohamed kama wanavyoonekana katika picha hiyo.

 VIONGOZI mbali mbali wa UVCCM pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdalla Juma Mabodi wakiomba dua katika Kaburi la Marehemu Mzee Abeid Amani Karume lililopo katika eneo la Afisi Kuu ya CCM Zanzibar.

MAKAMU Mwenyekiti wa UVCCM Taifa Tabia Maulid Mwita (kusho) Msimamizi na mwandaji wa Vipindi vya Shirika la Utangazaji Zanzibar ZBC Radio Suzan Kunambi (kulia) akimfanyia mahojiano kiongozi huyo kuputia kipindi cha Asubuhi na ZBC huko katika Studio za Shirika hilo Rahaleo Unguja.

NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.

NAIBU Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar Dk. Abdalla Juma Saadalla(Mabodi) amewahakikishia Umoja wa Vijana wa Chama hicho (UVCCM) kuwa ataendelea kushirikiana nao katika masuala mbali mbali ya kuwaletea wananchi maendeleo.

Ahadi hiyo ameitoa wakati akizungumza na viongozi wa UVCCM Taifa wakiongozwa na Mwenyekiti Kheir James na Makamu Mwenyekiti Tabia Maulid Mwita, waliofika Afisi Kuu ya CCM Zanzibar kwa ajili ya kutembelea na kuomba dua katika kaburi la aliyekuwa Rais wa kwanza wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar Marehemu Mzee Abeid Aman Karume .


Dk. Mabodi aliwambia viongozi hao kwamba kumbukumbu na historia ya Marehemu Mzee Abeid karume inatakiwa kulindwa na vijana wa CCM ambao wao ndio viongozi wa sasa na baadae wenye dhamana ya kulinda serikali na Chama visichukuliwe na wapinzani.


Naibu Katibu Mkuu huo amemtaja Marehemu Mzee Abeid Karume kuwa alikuwa ni kiongozi wa Mapinduzi mwenyekiti aliyekuwa na azna kubwa ya busara na falsafa pana ya masuala ya uongozi na ubunifu ndani na nje ya ASP na Serikali kwa ujumla.


 Amesema Afisi Kuu ya CCM Zanzibar inayoongozwa na Makamu Mwenyekiti Dk.Ali Mohamed Shein itatoa ushirikiano kwa UVCCM pamoja na jumuiya na taasisi zote za kisiasa na kiserikali ili wananchi waendelee kupata huduma bora za kijamii, kichumi na kisiasa.


 Pia, ameueleza msafara huo wa viongozi wa UVCCM waliofika Zanzibar kwa mara ya kwanza toka wachaguliwe kupitia Mkutano Mkuu wa Tisa wa Umoja huo Taifa, kwamba maendeleo yaliyopatikana visiwani Zanzibar yanatokana na juhudi za CCM kuisimamia Serikali itekeleze Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2015/2020.


“Kwanza karibuni sana Kisiwandui ambapo ndio sehemu pekee yenye historia na Ofisi za waasisi wetu wa Afro Shiraz Party (ASP), walioanzisha harakati za ukombozi wa Waafrika wa visiwa vya Zanzibar na hatimaye Januari 12, 1964 wakaung’oa utawala wa kisultani na kusimamisha Dola huru iliyojali maisha na utu wa watu wote.


Nyinyi vijana ni azna kubwa kwa chama chetu hivyo fanyeni kazi kwa ufanisi ili kulinda heshima na dhamana mnazopewa kwa lengo la kuwanufaisha vijana wenzenu ambao kwa njia moja ama nyingine hawajajaliwa kama zenu”, alisema Dk.Mabodi.


Naye Mwenyekiti wa UVCCM Taifa , Kheir James amekipongeza Chama cha Mapinduzi Zanzibar kwa juhudi zake za kuimarisha taasisi hiyo ya kisiasa licha ya kuwepo na changamoto za kisiasa zinazosababishwa na wapinzani.


Mwenyekiti Kheir amesema yupo tayari kufanya kazi na viongozi wa Chama cha Mapinduzi na Serikali kwa ujumla ili changamoto mbali mbali zinazowakabili vijana ziweze kupatiwa ufumbuzi wa kudumu na taasisi hizo.

 MAKAMU Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) Tabia Maulid Mwita ameishauri serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuongeza kasi katika usimamizi wa mamlaka zinazohusika na uendeshaji wa kesi za udhalilishaji wa kijinsia kwa wanawake, watoto na watu wenye ulemavu kuhakikisha zinatenda haki.


Kauli hiyo ameitoa leo wakati akizungumza katika kipindi Maalum kinachorushwa mubashara kila siku asubuhi na ridhaa ya Taifa ya Zanzibar ambayo ni Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC Radio) katika jengo la Shirika hilo lililopo Rahaleo Mjini Unguja.


Amesema miongoni mwa mikakati ya UVCCM ni kukemea vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia, dawa za kulevya pamoja na vitendo viovu vinavyosababisha mmomonyoko wa maadili kwa vijana.
Tabia ameeleza kuwa Umoja huo umejipanga kufanya kazi kwa bidii kwa lengo la kuharakisha maendeleo ya taasisi hiyo kisiasa na kiuchumi.


Amesema wakati wa vijana kutumiwa kama ngazi ya kufikia mafanikio kwa baadhi ya watu umekwisha na badala yake vijana hao watumie fursa zilizowazunguka kujitafutia kipato.


“ Vijana tunatumiwa na baadhi ya wanasiasa hasa inapokaribia kipindi cha kampeni za uchaguzi na wanapopata nafasi hawaanzishi miradi ya maendeleo ya kulisaidia kundi hilo ambalo wengi wao hawana ajira za uhakika.


Sasa ifikie wakati na sisi tuwe na misimamo kwa kujiajiri wenyewe kupitia sekta ya ujasiria mali na ufundi na watushauri mambo mbali mbali ya kuimarisha taasisi yetu kisiasa.


Kupitia kipindi hicho Makamu Mwenyekiti huyo ametoa wito kwa vijana wote nchini kuwaunga mkono viongozi wa Chama na Serikali hasa Mwenyekiti wa CCM Taifa Dkt. John Pombe Magufuli na Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein kwani viongozi wanaojali maslahi ya vijana.


Amesisitiza wananchi kuheshimu utawala wa kisheria kwa kuepuka uvunjaji wa sheria na miongozo mbali mbali ya nchi.


Pamoja na hayo amewataka viongozi wa UVCCM kuwa mfano wa kuigwa kivitendo, kauli, maadili, hekima na busara ili vijana wengine waliopo katika vyama vya upinzani wavutike na kujiunga na umoja huo.


 
Support : #BegaKwaBegaNaMamaSamia | JAK | CCM Arusha
Copyright © 2011. CCM Dijitali - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Jasper K
Proudly powered by Blogger
Link