Kwa ufupi
Kesi hiyo ilisimama kwa takribani muda wa miezi minne baada ya mahakama kukataa kupokea CD iliyotolewa na upande wa mashtaka dhidi ya Askofu Gwajima kama kielelezo cha ushahidi kwa kuwa hakijakidhi vigezo na upande wa mashtaka kukata rufaa dhidi ya uamuzi huo.
Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu itaendelea kusikiliza kesi ya kutoa lugha chafu inayomkabili Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima Josephat Gwajima ifikapo Septemba 29 mwaka huu.
Kesi hiyo ilisimama kwa takribani muda wa miezi minne baada ya mahakama kukataa kupokea CD iliyotolewa na upande wa mashtaka dhidi ya Askofu Gwajima kama kielelezo cha ushahidi kwa kuwa hakijakidhi vigezo na upande wa mashtaka kukata rufaa dhidi ya uamuzi huo.
Wakili wa Serikali, Jackqline Nyantori leo amemueleza Hakimu Mfawidhi wa mahakama hiyo, Cyprian Mkeha kudai kesi hiyo ilipaswa kuendelea kusikilizwa kwa ushahidi wa mashahidi wa upande wa mashtaka dhidi ya uamuzi wa kuikataa CD kuwa kielelezo cha ushahidi.
Hakimu Mkeha amesema kesi hiyo imekwisha simama kwa miezi minne haijasikilizwa hivyo aliwataka upande wa mashtaka kueleza kama wana nia ya kuondoa rufaa hiyo ili kuruhusu kesi kuendelea kusikilizwa ama la.