DKT. YONAZI AMELIKUMBUSHA JESHI
LA POLISI WAJIBU WA KUJIFUNZA
NA KUTOA ELIMU YA USALAMA
MTANDAO
Na Faraja Mpina na Chedaiwe Msuya, WHMTH, DODOMA
Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt. Jim Yonazi
amelikumbusha Jeshi la Polisi Tanzania kuwa linalo wajibu wa kujifunza na kuwaelimisha
wengine kuhusu makosa ya mtandao, namna ya kujilinda na kuchukua tahadhari dhidi ya
makosa ya mtandao.
Dkt. Jim ametoa rai hiyo wakati akifungua mafunzo ya usalama mtandao kwa Wakuu wa
Upelelezi wa Mikoa, Wakuu wa Vikosi na Wakuu wa madawati ya Upelelezi wa Jeshi la
Polisi kutoka Mikoa yote ya Tanzania Bara na Zanzibar yanayofanyika kwa siku tano jijini
Dodoma kuanzia tarehe 21 Machi hadi tarehe 25 Machi, mwaka 2022
Amesema kuwa, Jeshi la Polisi linalo wajibu wa kujifunza kila siku, kwa kuwa wao pia ni
washirika katika ulimwengu wa mtandao kupitia matumizi ya simu janja lakini pia Wimbo wa
Jeshi la Polisi unasema wazi kuwa wana jukumu la kulinda usalama na haki za wananchi
ambapo utekelezaji wa jukumu hilo unafanyika katika ulimwengu mpya wa kidijitali.
“Dunia inabadilika kuna uhalifu mwingi unaofanyika kwa njia ya mtandao na watu wa
makundi yote kwa kukusudia au bila kukusudia, hivyo watendaji mnapopatiwa elimu mna
wajibu wa kuelimisha wengine kupitia nafasi za utendaji mlizo nazo sasa”, Amezungumza
Dkt. Yonazi
Ameongeza kuwa,“Ukimchapa mtoto lazima umfahamishe kwanini umemchapa na kosa ni
lipi, vivyo hivyo kwenye makosa ya mtandao, kabla ya kuyashughulikia ni vema wananchi
wapatiwe elimu na kufahamu makosa ya mtandao ni yapi”.
Dkt. Yonazi ameyazungumzia mafunzo hayo kuwa yanatoa taswira nzima na uelekeo wa
nchi katika kushughulikia masuala ya usalama mtandao ili kufikia malengo yanayotarajiwa
huku wajibu wa Wizara hiyo ni kuhakikisha mafunzo hayo ni endelevu na usalama katika
mtandao unasimamiwa vizuri.
Akizungumza na hadhira hiyo Mkuu wa Upelelezi na Makosa ya Jinai nchini (DCI) CP
Camilius Wambura ameishukuru Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
kwa kuwezesha mafunzo hayo, kwa kuwa yatawasaidia watendaji wa Jeshi la Polisi
Tanzania kuongeza ujuzi utakaowafungua zaidi na kupanua wigo wa kupambana na uhalifu
hasa wa makosa mtandao.
“Teknolojia inabadilika kila kukicha hivyo mafunzo ya mara kwa mara kwa watendaji wetu
yanahitajika ili kuendana na kasi ya mabadiliko haya kwa watendaji kupitishwa wapi tulipo
na wapi tunaelekea katika kukabiliana na uhalifu wa mtandao”. Amezungumza Wambura
Naye Mkaribu Mwandamizi wa Polisi, SSP Joshua Mwangasa ameishukuru Serikali kupitia
Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kwa kuwajengea uwezo watendaji
wa Jeshi la Polisi nchini pamoja na hatua zinazoendelea za kuanza ujenzi wa maabara za
uchunguzi wa kisayansi zitakazojengwa kikanda katika mikoa sita ya Mbeya, Arusha
Dodoma, Dar es Salaam, Mwanza na Zanzibar ambazo zitasaidia kupanua wigo wa
uchunguzi wa makosa ya mtandao.
Mafunzo hayo ya usalama mtandao yanatolewa kwa watendaji wapatao 100 wa Jeshi la
Polisi Tanzania ikiwa ni muendelezo wa mafunzo yaliyotolewa mwezi Februari mwaka huu
kwa watendaji wa ngazi ya chini ya Jeshi hilo na sasa ni zamu ya wasimamizi wao ambao ni
Wakuu wa Upelelezi wa Mikoa, Wakuu wa Vikosi kama vile TAZARA na Bandari, Wakuu wa
Madawati ya Upelelezi wa Mikoa na Wakufunzi wa vyuo vya Polisi nchini.
Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari



