Home » » HATUTAWASHUSHA VYEO TU BALI MTAONDOLEWA KWENYE UTUMISHI WA UMMA’ BASHUNGWA

HATUTAWASHUSHA VYEO TU BALI MTAONDOLEWA KWENYE UTUMISHI WA UMMA’ BASHUNGWA

Written By CCMdijitali on Thursday, March 31, 2022 | March 31, 2022


  

HATUTAWASHUSHA VYEO TU BALI

 MTAONDOLEWA KWENYE 

UTUMISHI WA UMMA’ BASHUNGWA


OR-TAMISEMI

Waziri Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mhe. Innocent Bashungwa
amesema hatawafumbia macho watumishi ambao hawatoshi na kuwa wataondolewa kwenye utumishi wa umma na si kuwashusha vyeo au kuwahamisha

Pia Mhe. Bashungwa amewataka watumishi katika Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kufanya kazi kwa bidii, kujituma na uadilifu mkubwa na kwa wachache wanaoenda kinyume na taratibu hizo watachukuliwa hatua kwa kutolewa kwenye utumishi wa umma.

Amesema kumekuwepo na utaratibu wa kuwashusha vyeo watumishi wachache ambao wanafanya kazi kwa mazoea na kutozingatia taratibu za kiutumishi lakini chini ya usimamizi wangu hilo jambo halivumiliki watatolewa kwenye utumishi wa umma maana wanadhohofisha mchakato mzima wa kuleta maendeleo kwa Watanzania.

Mhe. Bashungwa ametoa wito huo 29, Machi 2022 alipozungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma muda mfupi baada ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan kuiagiza Ofisi ya Rais TAMISEMI kuzisimamia Halmashauri ipasavyo na kuchukua hatua kwa watumishi wenye matumizi mabaya ya fedha za Serikali.

“Nimuhakikishie Mheshimiwa Rais kwa maagizo aliyoyatoa leo kuhusu weledi na uadilifu wa Watumishi wa umma, nitaanzia hapa Ofisi ya Rais TAMISEMI kuhakikisha tunajenga taswira na mwelekeo unaoendana na ofisi ya Mheshimiwa Rais” amaesema Bashungwa


Amesema matarajio yake ni kuona wale wachache waliokuwa wanaenda kinyume wanabadilika na kujirekebisha maana kuna Watanzania wasomi na wazalendo wapo mtaani ambao wakipewa nafasi wataweza kutumikia Watanzania kwa uaminifu.

Aidha, Waziri Bashungwa amemwagiza Katibu Mkuu Ofisi ya Rais TAMISEMI ndani ya siku tatu kuhakikisha anamaliza uchambuzi wa Wakahazina wa Halmashauri ambao hawafanyi kazi kikamilifu ili waweze kuchukuliwa hatua.

Pia, Waziri Bashungwa amewataka Wakuu wa Mikoa na Wilaya kuhakikisha wanasimamia nidhamu ya Utumishi katika maeneo yao hasa katika usimamizi wa fedha za utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuchukua hatua mapema kabla ya Wizara haijalazimika kufanya hivyo.

Share this article :
 
Support : #BegaKwaBegaNaMamaSamia | JAK | CCM Arusha
Copyright © 2011. CCM Dijitali - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Jasper K
Proudly powered by Blogger
Link