MWELEKEO WA KAZI, AJIRA, VIJANA NA
WENYE ULEMAVU BAADA YA MWAKA
MMOJA WA RAIS SAMIA WABAINISHWA
Ofisi
ya Waziri Mkuu- Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu imebainisha
mipango mikakati ya kiutendaji katika majukumu inayoyaratibu ili
kuhakikisha Maelekezo ya Mhe. Rais na Mhe. Waziri Mkuu yanatekelezwa
kwa ufanisi na weledi katika kuboresha huduma za Ofisi hiyo, baada ya
mwaka mmoja wa serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Samia
Suluhu Hassan.
Akieleza mwelekeo wa Ofisi hiyo, kwa waandishi wa
habari leo jijini Dar es salaam, tarehe 20 Machi, 2022, Mhe. Naibu
Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu), Mhe.
Patrobas Katambi, amefafanua kuwa pamoja na kuwa Ofisi hiyo imetekeleza
kwa mafanikio majukumu yake, hatua inayofuata ni kujikita katika tafiti
katika masuala inayoratibu ya kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu.
Mhe.
Katambi amefafanua kuwa Mhe. Rais amewataka waandae Programu maalum ya
kutengeneza fursa za Ajira kwa vijana, ambapo Programu hiyo itahusisha
Wizara, Idara, Wakala na Taasisi zote za serikali, Sekta Binafsi.
Programu hiyo itahakikisha kuwa kila fedha inayotokana na serikali kwa
hapa ndani au tunazozipata kutoka nje ya nchi, iweze kuzalisha fursa za
ajira kwa vijana waliojiajiri au kutengeneza ajira. ” Amesisitiza
Katambi
Ameongeza kuwa Programu hiyo itajikita pia katika katika
miradi mikubwa ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali, ambapo utekezaji
wa miradi hiyo utaweza kuzalisha ajira za moja kwa moja na ambazo sio
za moja kwa moja.
Amefafanua kuwa mkakati mwingine ambao Ofisi
hiyo iliyonao ni kuzitafuta Taasisi na wadau wa kimaendeleo watakao weza
kutoa ruzuku, misaada pamoja na fedha zitakazo wawezesha vijana
kujiajiri. Aidha, ameongeza kuwa wamejipanga kufanya Ufuatiliaji wa
fedha zinazotolewa na halmashauri kwa ajili ya kuwakopesha Wanawake,
Vijana na Wenye Ulemavu ambapo hadi sasa, zaidi ya shilingi bilioni
145.8 zimetolewa kote nchini.



