Home » » WAZIRI WA AFYA MHE MHAGAMA AMTAMBULISHA MGOMBEA MTEULE WA SHIRIKA LA AFYA DUNIANI KWA WAANDISHI WA HABARI

WAZIRI WA AFYA MHE MHAGAMA AMTAMBULISHA MGOMBEA MTEULE WA SHIRIKA LA AFYA DUNIANI KWA WAANDISHI WA HABARI

Written By CCMdijitali on Saturday, March 22, 2025 | March 22, 2025

HOTUBA YA MHESHIMIWA WAZIRI WA AFYA, JENISTA MHAGAMA KWA WAANDISHI WA HABARI WAKATI WA KUMTAMBULISHA PROF. MOHAMED YAKUB JANABI KAMA MGOMBEA MTEULE WA NAFASI YA UKURUGENZI WA SHIRIKA LA AFYA DUNIANI (WHO) KANDA YA AFRIKA UTAKAOFANYIKA TAREHE 18 MEI 2025, GENEVA, USWISI.

Katibu Mkuu Wizara ya Afya – Dkt. Seif Shekalaghe

Kaimu Mganga Mkuu wa Serikali –

Mshauri wa Rais wa Masuala ya Afya na Lishe na Mkurugenzi Mtendaji Hospitali ya Taifa Muhimbili – Prof. Mohamed Janabi.

Mkurugenzi Huduma za Kinga na Mkurugenzi Mkuu wa Jumuiya ya Afya ya Afrika Mashariki, Kati na Kusini (ECSA – HC) – Dkt. Ntuli A. Kapologwe

Wageni Waalikwa mliopo hapa

Ndugu Wanahabari:

Nawasalimu kwa jina la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania…

Mnamo tarehe 14 Januari 2025 Shirika la Afya Duniani Kanda ya Afrika liliitisha kikao maalum na nchi wanachama wake 47 kwa ajili ya kujadili uchaguzi wa Mkurugenzi wa Shirika hilo kwa Kanda ya Afrika.

Ikumbukwe mnamo mwezi Agosti 2024, Tanzania iliwania nafasi hii kupitia Marehemu Dkt. Faustine E.Ndugulile aliyekuwa pia alikuwa Mbunge wa Jimbo la Kigamboni. Dkt. Ndugulile alishinda nafasi hiyo katika uchaguzi uliofanyika mnamo tarehe 26 Agosti 2024 wakati wa Mkutano wa 74 wa Shirika la Afya Duniani Kanda ya Afrika uliofanyika Brazaville, Jamhuri ya Kongo.

Dkt. Faustine alishinda nafasi hiyo baada ya kuwashinda wagombea wengine watatu ambao ni Dkt. Socce Fall (Senegal), Dkt. Richard Mihigo (Rwanda) na Dkt. Boureima Hama Sambo (Niger).



Ndugu Wanahabari;

 

Tarehe 27 Novemba 2024, Tanzania na Jumuiya ya Kimataifa tulipokea kwa mshutko mkubwa taarifa za kifo cha mpendwa wetu Dkt. Faustine Ndugulile ambaye alifariki kabla ya kuanza kuitumikia nafasi hiyo Mwezi Februari 2025. Naomba tusimame kwa dakika moja kumuombea Marehemu Dkt.Faustine Ndugulile apumzike kwa amani.

 

Ndugu Wanahabari:

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwa ni miongoni mwa nchi wanachama wa Shirika la Afya Duniani Kanda ya Afya ilimpendekeza Prof. Mohamed Yakub Janabi, Mshauri wa Rais kwenye Masuala ya Afya na Lishe ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kuwania nafasi ya Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani Kanda ya Afrika.

Kama mnavyofahamu, Shirika la Afya Duniani ni chombo yenye mchango mkubwa katika kuboresha mifumo ya afya ulimwenguni. Nafasi hii ya Ukurugenzi wa Kanda ya Afrika ni muhimu sana kwa sababu inatoa mwelekeo wa kisera, kisayansi, na kimkakati katika kutatua changamoto za afya zinazolikabili bara letu, hivyo tunaamini Tanzania kuwa na mwakilishi katika Shirika hili itaweza kuongeza mchango wake katika maendeleo ya Sekta ya Afya barani Afrika.

Ndugu Wanahabari;

Prof. Mohamed Janabi ni mtaalamu mwenye uzoefu mkubwa katika sekta ya afya. Amehudumu katika nyadhifa mbalimbali za uongozi, ikiwa ni pamoja na kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili ambapo ameshiriki katika kuleta mageuzi makubwa ya utoaji wa huduma bora za afya na kuimarisha mifumo ya rufaa kutoka vituo vya kutolea huduma za afya ngazi ya msingi mpaka Taifa.

Akiwa Mkurugenzi Mtendaji wa kwanza na mwanzilishi wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Janabi aliongoza mageuzi makubwa katika huduma za matibabu ya moyo nchini Tanzania na Barani Afrika na hivyo kupekelea kupunguza rufaa za nje ya nchi kwa asilimia 95.

Pamoja na sifa hizo mbili, Prof. Janabi amekuwa akishiriki kwenye masuala ya utekelezaji wa afua za afya ya jamii kwa kutoa elimu ya afya na kushiriki kwenye shughuli mbalimbali za uimarishaji huduma za afya ngazi ya jamii. Prof. Janabi ameshiriki kwenye tafiti mbalimbali zilizolenga kuboresha utoaji wa huduma za afya pia ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Tiba na Afya Shirikishi Muhimbili (MUHAS) na Mhadhiri wa kualikwa katika Vyuo mbalimbali Duniani.

Prof. Janabi amefanya kazi kwa ukaribu na Mashirika ya Kikanda, Kimataifa, Serikali mbalimbali pamoja na Wadau wa Sekta ya Afya ili kuboresha upatikanaji wa huduma bora na endelevu za afya kwa wananchi. Uzoefu wake wa kitaaluma na kiutendaji unampa sifa zinazohitajika kuongoza Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika kwa ufanisi.

Ndugu Wanahabari;

Baadhi ya vigezo vilivyopelekea Prof.Janabi kugombea nafasi hii ni pamoja na;

v Uongozi Thabiti,

Prof. Janabi, ameonesha uwezo mkubwa wa kuleta mageuzi katika Sekta ya afya kupitia uongozi wake kwenye taasisi alizoziongoza lakini pia kuwa Mshauri Mkuu wa Masuala ya Afya na Lishe kwa Waheshimiwa Marais wawili (Mhe. Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete na Mhe. Dkt. Samia Suluh Hassan).

 

v Uwezo wa Kitaalamu,

Prof. Janabi kupitia tafiti alizozifanya ndani na nje ya Nchi zimemjengea uelewa mpana wa masuala ya Afya ya Jamii na Lishe na kufanikiwa kuleta mabadiliko ya Sekta ya Afya nchini.

 

v Mtazamo wa Kikanda na Kimataifa,

Prof. Janabi ana mtazamo na maono ya maendeleo ya Sekta ya Afya yanayozingatia afya kwa wote na hii inatokana na uzoefu wake wa kufanya kazi katika maeneo tofauti ndani na nje ya nchi.

 

v Ushirikiano na Wadau wa Sekta ya Afya na Lishe,

Prof. Janabi ameendelea kuwa na uhusiano mzuri na mashirika ya Kikanda na Kimataifa, Taasisi za utafiti, na wahisani wa Afya ambayo kwa ujumla yanalenga kuimarisha mifumo ya Afya.

Ndugu Wanahabari;

Prof. Janabi anaingia katika uchaguzi huu akishindana na wagombea wengine wanne ambao ni: Profesa Moustafa Mijiyawa (Togo), Dkt. Michael Yao (Ivory Coast), Dkt. Boureima Hama Sambo (Niger) na Dr. Mohamed Lamine Drame (Guinea Conakry).

Wagombea hawa wanaowania nafasi hii pamoja na Prof. Janabi wote wanatokea nchi za Afrika ya Magharibi na wawili kati yao Dkt. Michael Yao (Ivory Coast) na Dkt. Boureima Hama Sambo (Niger) walishiriki katika uchaguzi uliopita ambao Marehemu Dkt. Ndugulile alishinda.

Ndugu Wanahabari;

Tanzania kupitia mgombea wetu Prof. Janabi tunaimani kubwa ya kushinda tena kwenye uchaguzi wa Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani Kanda ya Afrika kutokana na sababu zifuatazo:-

v Historia, Diplomasia pamoja na Ushirikiano ambao Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameendelea kuuimirisha baina ya nchi yetu na mataifa mengine, zinaipaisha Taifa letu kwenye majukwaa ya Kikanda na Kimataifa.

 

v Taifa letu lina sifa ya kutoa viongozi wenye weledi katika nyanja mbalimbali, na tunajivunia kwamba Prof. Janabi yuko tayari kulihudumia Bara letu katika nafasi hii.

 

v Uzoefu wa Prof. Janabi katika masuala ya ugharamiaji wa huduma za afya kwa kuzingatia kipindi hiki ambacho Dunia inapita katika changamoto ya kuwa na vyanzo vya uhakika wa ugharamiaji wa huduma za afya; uzoefu wake katika kudhibiti na kupambana na magonjwa ya mlipuko, uzalishaji wa bidhaa za afya nchini pamoja na usimamiaji wa mifumo ya utoaji wa huduma za afya zinatupa nafasi kubwa ya kushinda nafasi hii.

Ndugu Wanahabari;

Kampeni za wagombea wa nafasi hii tayari zimeshaanza kwa njia mbalimbali, nasi hatuna budi kushirikiana kumnadi mgombea wetu kwa nguvu, ari na morari kubwa. Nitoe rai kwa wananchi, mashirika na wadau wa Sekta wa ndani na nje kuungana pamoja katika kumnadi na kumuombea dua mgombea wetu.

Tuna imani kuwa kwa uongozi wake, Afrika itapiga hatua kubwa katika kuboresha mifumo ya afya, kupambana na magonjwa, na kuhakikisha kila mwananchi anapata huduma bora za afya.

Mungu ibariki Tanzania! Mungu ibariki Afrika! Asanteni kwa kunisikiliza.

 Published from Blogger Prime Android AppPublished from Blogger Prime Android App

Share this article :
 
Support : #BegaKwaBegaNaMamaSamia | JAK | CCM Arusha
Copyright © 2011. CCM Dijitali - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Jasper K
Proudly powered by Blogger
Link