Home » » Shamra shamra za maadhimisho ya sherehe za kutimia Miaka 54 ya Mapinduzi ya Zanzibar zaendelea.

Shamra shamra za maadhimisho ya sherehe za kutimia Miaka 54 ya Mapinduzi ya Zanzibar zaendelea.

Written By CCMdijitali on Tuesday, January 9, 2018 | January 09, 2018

 Wanafunzi wa Skuli za Msingi na Sekondari wa Wizaya Chake Chake Pemba wakishuhudia hafla ya uzinduzi wa Jengo Jipya la Baraza la Mji Chake Chake Pemba.

 Baadhi ya Wananchi waliohudhuria Uzinduzi wa Jengo Jipya la Baraza la Maji Chake chake Pemba katika shamra shamra za maadhimisho ya kutimia Miaka 54 ya Mapinduzi ya Zanzibar.

 Balozi Seif akizungumza na Wananchi na Watumishi wa Baraza la Mji Chake Cheka wakati wa hafla ya kulizindua Jengo Jipya la Baraza hilo ikiwa ni shamra shamra za Miaka 54 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.
Kushoto ya Balozi Seif ni Waziri wa Fedha na Mipango wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Dr. Khalid Salum Mohamed.
 
 Haiba ya Jengo Jipya la Baraza la Mji wa Chake Chake linavyoonekana katika maeneo ya kando ya Bara bara ya Mji wa Chake kuelekea Macho Mane.


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akizindua rasmi Jengo Jipya la Baraza la Maji Chake chake Pemba ikiwa ni shamra shamra za maadhimisho ya sherehe za kutimia Miaka 54 ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Picha na – OMPR – ZNZ.

                                        Press Release:-

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar haitamuonea haya  kwa kumfukuza kazi mara moja Mtumishi yeyote wa Serikali au Taasisi za Umma atakayegundulika anatoa huduma  kwa Umma katika misingi ya Kibaguzi.

Akizindua rasmi Jengo Jipya la Ofisi ya Baraza la Mji la Chake chake Pemba ikiwa miongoni mwa shamra shamra za sherehe za Maadhimisho ya kutimia Miaka 54 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar  Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema Serikali Kuu inataka kuona mabadiliko makubwa katika maeneo ya Utawala.

Balozi Seif alisema Serikali imefanya mageuzi makubwa katika mfumo uitwayo Ugatuzi na kuhamisha majukumu yake katika Serikali za Mitaa kwa lengo la kuimarisha utoaji bora wa huduma mbali mbali kwa Wananchi.

Alisema uhamishaji huo wa majukumu umeanza rasmi Mwaka huu unaoendelea wa Fedha ambapo huduma za msingi kama vile elimu ya maandalizi na Msingi, afya ikiwemo huduma za msingi  za Kilimo sasa ziotakuwa chini ya dhamana ya Serikali za Mitaa za maeneo husika.

Alieleza kwamba Wananchi wanapaswa kutambua kuwa kitendo hicho cha kuwapelekea huduma karibu yao na huduma hizo zikatolewa katika mazingira mazuri mfano wa Jengo hilo zina lengo la kuimarisha  Utawala wa Demokrasia  hapa Nchini.

Balozi Seif alifahamisha kwamba wakati Serikali Kuu itabakia na mambo ya jumla kama vile uandaaji wa sera, kanuni na usimamizi wa jumla uimarishaji huo wa Serikali za Mitaa unatoa nafasi na fursa pana kwa Wananchi wajiongoze na kujitawala wenyewe katika maamuzi ya mambo yanayowakabili wenyewe.

Aliwakumbusha Wananchi kwamba Madiwani waliowachagua  wanawajibika kwao Wananchi, na pale watakapoona huduma wanazopaswa kupewa haziendi vyema wana haki ya kuwawajibisha, kuwahoji sambamba na kutaka maelezo yatakayowaridhiosha huku wakielewa kwamba hiyo ndio maana ya kuimarisha Demokrasia.

Hata Balozi Seif aliwaomba Wananchi waelewe kuwa kujitawala kuna gharama zake ambazo hazina budi kulipwa na Wananchi wenyewe wanaojitawala huku wakielewa kwamba Baraza la Mji ni lao linalotoa huduma kwao ambazo ni gharama zinazotokana na ada wanazotowa.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alielezea kutofurahishwa kwake na taarifa za Machinjio ya Wesha yasiyotumika vizuri na kuachwa bila ya matunzo jambo ambalo halikubaliki na wahusika wanapaswa kulishughulikia mara moja.

Balozi Seif  alionya kwamba wakati atalifuatilia suala hilo lazima Wananchi na watumishi wa Mabaraza la Miji  wathamini mali wanazopatiwa ambazo hugharimu fedha nyingi na kuwataka Wananchi wa Chake wakatae kuona mali zao zinatumika ovyo na hatimae kuharibika mapema.

Akitoa Taarifa za ujenzi wa Jengo hilo la Baraza la Mji wa Chake Chake Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Nd. Khamis Mussa Omar  alisema ujenzi huo ni sehemu ya Mradi Mkuu wa Huduma za Jamii  Zanzibar { ZUSP }.

Ndugu Mussa alisema changamoto ya ujenzi huo ilitokana na ubovu wa Nguzo za asili ambazo Mkandarasi wa Mradi huo alilazimika kujenga upya nguzo hizo na kuongezeka kwa gharama za ujenzi huo zilizofikia asilimia 36.4%.

Alisema mradi huo Mkuu wa huduma za Jamii hadi kukamilika kwake unatarajiwa kugharimu jumla ya shilingi Bilioni Moja ambapo tayari kwa awamu ya kwanza  zimeshajengwa Ngazi Nane za Kuvukia Wananchi kutoka sehemu moja kwenda nyengine katika maeneo ya Mabondeni.

Katibu Mkuu Mussa aliishukuru Benki ya Dunia { World Bank } kwa kuendelea kuipatia Mikopo  ya Fedha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili kutekeleza miradi mbali mbali ya Maendeleo.

Naye Waziri wa Fedha na Mipango Zanzibar Dr. Khalid Salum Mohamed  akimkaribisha Balozi Seif  kwenye Hafla hiyo alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inakusudia kuweka Taa za Bara barani katika Miji yote Mitatu ya Kisiwa cha Pemba. 

Dr. Khalid alisema jumla ya Dola za Kimarekani 55 Milioni zitakazotolewa Mkopo na Benki  ya Dunia zitaelekezwa katika mradi huo muhimu kwa kustawisha Miji hizo sambamba na kuweka haiba nzuri ya maeneo hayo.

Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kustawisha maisha ya Wananchi wake kadri ya hali ya uchumi inavyozidi kuongezeka mfano wa Mwaka 2016 uliopata mafanikio makubvwa kutokana na kuongezeka kwa Pato la Taifa na kufikia hadi asilimia 6.8%.

Waziri Khalid alifahamisha kwamba nyongeza za Mishahara zilizotolewa na Serikali zikaenda sambamba na upandishwaji wa Pencheni kwa Wazee waliostaafu na wale waliofikia umri zaidi ya Miaka 70 ni miongoni mwa mafanikio ya ongezeko hilo la Mapato ya Taifa.


Othman Khamkis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
9/1/2018.

Share this article :
 
Support : #BegaKwaBegaNaMamaSamia | JAK | CCM Arusha
Copyright © 2011. CCM Dijitali - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Jasper K
Proudly powered by Blogger
Link