Home » » SERIKALI YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR KUTOA USHIRIKIANO UTEKELEZAJI WA MFUMO WA ANWANI ZA MAKAZI

SERIKALI YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR KUTOA USHIRIKIANO UTEKELEZAJI WA MFUMO WA ANWANI ZA MAKAZI

Written By CCMdijitali on Wednesday, February 9, 2022 | February 09, 2022

 

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla

 







Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itatoa kila aina ya ushirikiano ili kufanikisha Utekelezaji wa Mfumo wa Anwani za Makazi.

Mhe. Hemed ameeleza hayo wakati akitoa Salamu katika kikao kazi cha Wakuu wa Mikoa kuhusu Utekelezaji wa Mfumo wa Anwani za Makazi kilichofanyika Ukumbi wa Jakaya Kikwete Convention Centre Jijini Dodoma.

Amesema kukamilika kwa mfumo huo ni tija kwa Taifa ambapo itasaidia kuweza kufikia dhamira ya Serikali ya kuwa na Maendeleo endelevu.

Aidha Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amesema kukamilika kwa zoezi hilo itasaidia kurahisisha zoezi la Sensa ya Watu na Makazi inayotarajiwa kufanyika mwezi Agosti mwaka huu ambapo kukamilika kwa zoezi hilo  kutasaidia Makarani wa Sensa hiyo wataweza kutumia mfumo huo kwa kuwaongoza kuwafikia wananchi kwa urahisi zaidi.

Sambamba na hayo Mhe. Hemed ameeleza kuwa Zoezi la Mfumo wa Anwani za Makazi ni la kihistoria ambapo ni vyema kwa wahusika na wataalamu kwa ujumla kuzingatia maelekezo wanayopewa ili kufanya kazi kwa ufanisi zaidi.

Kikao hicho kimeongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan na kuhudhuriwa na viongozi mbali mbali akiwemo Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt Philip Isdor Mpango,  Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.  Kassim Majaliwa Majaliwa, Mawaziri kutoka SMT na SMZ, Wakuu wa Mikoa na viongozi mbali mbali wa Serikali.

Imetolewa na Kitengo cha Habari (OMPR)
08 Februari 2022

Share this article :
 
Support : #BegaKwaBegaNaMamaSamia | JAK | CCM Arusha
Copyright © 2011. CCM Dijitali - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Jasper K
Proudly powered by Blogger
Link