WAZIRI MKUU AKUTANA NA UJUMBE WA WAFANYABIASHARA KUTOKA FALME YA SAUDI ARABIA
▪️Awaeleza mikakati ya Tanzania katika kuvutia wawekezaji.
▪️Awakaribisha kuwekeza kwenye Sekta ya Nishati
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali itaendelea kuweka mazingira bora ya uwekezaji nchini ili kuendelea kuwavutia wawekezaji.
Ameyasema hayo leo, (Jumatano 12 Februari 2025) alipokutana na Ujumbe wa Wafanyabiashara kutoka Falme ya Saidi Arabia, Katika Ofisi ndogo ya Waziri Mkuu magogoni jijini Dar es Salaam.
Mheshimiwa Majaliwa amesema uhusiano baina ya Tanzania na Saudi Arabia umeendelea kuimarika na kufungua fursa kwa wawekezaji kutoka Saudi Arabia kuwa na wigo wa kuwekeza nchini Tanzania hususan katika sekta za nishati, Kilimo, Viwanda, Mifugo Utalii na biashara.
Aidha, amesema Tanzania imeendelea kunufaika na fursa ya kusafirisha bidhaa za mazao na mifugo kwenda nchini Saudi Arabia jambo ambalo limeendelea kukuza uchumi wa nchi.
Katika hatua nyingine, Mheshimiwa Majaliwa ametoa wito kwa wawekezaji hao kuwekeza katika sekta ya nishati ili kuongeza nguvu katika kampeni ya nishati safi ya kupikia iliyoanzishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.
“Serikali yetu imeweka mkazo katika kufikia malengo ya kuwawezesha wananchi kutumia nishati safi ya kupikia na kuepukana na matumizi ya nishati zisozo rafiki kwa mazingira, Nchi yetu bado ina fursa nyingi za uwekezaji katika sekta ya nishati. Ninawakaribisha sana.”
Kwa Upande Wake, Rais wa Chemba ya Biashara wa Falme ya Saudi Arabia, Mheshimiwa Hassan Bin Moejeb Al Huwaizi, amesema yeye pamoja na Ujumbe wake wanaipongeza Serikali ya Tanzania kwa kuwavutia wawekezaji hususan kutoka Nchini Saudi Arabia.