WATENDAJI ARDHI WATAKIWA KUTOCHELEWESHA HUDUMA KWA MAKUSUDI
Na Munir Shemweta, WANMM IRINGA Serikali imewataka watendaji wa sekta ya Ardhi nchini kutochelewesha huduma za sekta ya Ardhi kwa mak...
WATENDAJI ARDHI WATAKIWA KUTOCHELEWESHA HUDUMA KWA MAKUSUDI
Written By CCMdijitali on Saturday, February 1, 2025 | February 01, 2025
Na Munir Shemweta, WANMM IRINGA
Serikali imewataka watendaji wa sekta ya Ardhi nchini kutochelewesha huduma za sekta ya Ardhi kwa makusudi wakati wanapowahudumia wananchi wanaokwenda kupata huduma katika ofisi zao.
Hayo yameelezwa Januari 31, 2025 mkoani Iringa na Mkurugenzi wa Upimaji na Ramani wa Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Bw. Hamdouny Mansoor wakati wa kikao kazi cha watumishi wa sekta ya Ardhi Mkoa wa Iringa.
Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Mhandisi Anthony Sanga, Bw. Mansoor amesema kumekuwa na ucheleweshaji huduma kwa makusudi na wakati mwingine watendaji wa sekta ya Ardhi kuwatuma mwananchi wanaokwenda kupata huduma.
"Sasa anakuja mwananchi anasema anataka kulipa kodi anaelezwa, aah hiyo kazi ni ya Afisa Ardhi nenda kulee mimi mpima, si umuelekeze tu, wakati mwingine tunatoa kauli ambazo siyo nzuri kwa wananchi wanaofika kupata huduma za Ardhi kwenye ofisi zetu" amesema.
Aidha, Mansoor kupitia kikao hicho kilichoandaliwa na Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Iringa ametaka kuwekwa utaratibu rasmi katika ofisi zote za Ardhi kuanzia ngazi ya wilaya wa namna ya kupata hati ili wananchi wauelewe na kuufuata utaratibu huo.
"Inasisitizwa ili upate hati ni vitu gani vya msingi vinatakiwa viwepo kwa wananchi kupata hati yake, viainishwe na vibandikwe katika ofisi zetu za ardhi" amesema.
Kwa upande wake Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Iringa Bw. Frank Minzikuntwe ameeleza kuwa, kikao kilichofanyika cha watumishi kilikuwa na lengo la kuzungumza na kupeana mikakati pamoja na mipango kazi ya namna ya kushughulikia kero na utoaji huduma za sekta ya ardhi kwa haraka zaidi.
"Sisi kama watendaji wa sekta ya Ardhi katika mkoa wa Iringa tunaahidi watumishi wote katika ngazi ya mkoa tutafanya kazi kwa weledi na uaminifu na kuwahudumia wananchi kwa tija ili waweze kupata huduma kwa wakati unaostahili’’. amesema
Kikao hicho cha siku moja kimeshirikisha watendaji wa sekta ya ardhi kutoka halmashauri zote za mkoa wa Iringa pamoja na wale wa Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi mkoa wa Iringa.
Sehemu ya watumishi wa sekta ya ardhi mkoa wa Iringa wakifuatilia majadiliano wakati wa kikao kazi cha watumishi wote wa sekta ya ardhi mkoa wa Iringa kilichofanyika jana. |
Kamishna wa Ardhi Msaidizi mkoa wa Iringa Bw. Frank Minzikuntwe akizungumza katika kikao kazi cha watumishi wa sekta ya ardhi mkoa wa Iringa jana. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI) |
Sehemu ya watumishi wa sekta ya ardhi mkoa wa Iringa wakifuatilia majadiliano wakati wa kikao kazi cha watumishi wote wa sekta ya ardhi mkoa wa Iringa kilichofanyika jana. |
THBUB YATEMBELEA VYUO VYA MAFUNZO YA AMALI, PEMBA
THBUB YATEMBELEA VYUO VYA MAFUNZO YA AMALI, PEMBA
TUME ya Haki za Binaadamu na Utawala Bora (THBUB) imefanya ziara ya kuvitembelea vyuo
viwili vya Mafunzo ya Amali vya Vitongoji, Wilaya ya Chake Mkoa wa Kusini Pemba na cha
Daya Mtambwe, Wilaya ya Wete, Mkoa wa Kaskazini Pemba, kwa lengo la kutoa elimu na
kujenga uelewa mpana kwa jamii juu ya dhana nzima ya Haki za Binadamu na Misingi ya
Utawala Bora.
Maafisa wa Tume hiyo, Ofisi ya Pemba wakiongozwa na Afisa Uchunguzi Ndg. Ramadhani Slaa
wameifunza jamii juu ya umuhimu wa kutambua Haki za Binaadamu na Utawala Bora pamoja
ushiriki na kuanzisha klabu za Haki za Binaadamu katika vyuo na kuwashauri wanafunzi wa vyuo
hivyo kujiunga na klabu hizo.
Akizungumza kwenye ziara hiyo, ofisi za chuo cha Vitongoji, Bw. Slaa alieleza nia ya ziara yao
chuoni hapo mbali na kutoa elimu ya Haki za Binaadamu na Utawala Bora lakini kushirikiana na
vyuo hivyo kuanzisha Klabu za Haki za Binadamu na Utawala Bora ili kukuza ushirikiano na nguvu
ya pamoja kwa kuongeza uelewa kwa jamii juu dhana ya Haki za Binaadamu na misingi ya Utawala
Bora.
Aidha, Bw. Ramadhan Slaa awasihi wanafunzi vyuoni humo kuendelea kuwa mabalozi wazuri wa
jamii zao katika kueneza dhana halisi ya Haki za Binaadamu na misingi ya Utawala Bora ili kukuza
jamii yenye uelewa mpana kwa maeneo hayo.
Katika hatua nyengine, THBUB ilimshauri, Mkuu wa chuo cha Daya cha Mtambwe, Mwl. Saada Ali
Hamad, kuanzisha Klabu ya Haki za Binadamu na Utawala Bora chuoni hapo ili kuongeza hamasa
na uelewa zaidi kwa jamii.
Naye, Mwalimu dhamana wa Chuo cha Mafunzo ya Amali cha Vitongoji na Mkuu wa Idara ya
Masomo Mtambukwa chuoni hapo, Mwl. Khamis Abdalla Khamis alitoa shukrani kwa THBUB kwa
kuwatembelea chuoni hapo sambamba na kuishauri Tume kuwa karibu na Klabu hizo ili kuzijengea
uimara na ziwe endelevu pamoja na kuahidi kuzisimamia vyema katika kuendeleza shughuli za
kutoa elimu kupitia klabu hizo.
Halikadhalika,kwa nyakati tofauti wanafunzi wa vyuo viwili hivyo, walipata nafasi ya kuuliza maswali
kuhusu dhana na uelewa wa Haki za Binaadamu na Utawala Bora pia kutaka kujua umuhimu na
faida za kujiunga na Klabu za Haki za Binadamu na Utawala Bora vyuoni humo.
Kwaupande mwengine, wanafunzi hao wameiomba THBUB kurudi tena kwenye vyuo vyao na
kujenga utamaduni wa kuwatembelea mara kwa mara ili wajifunze zaidi. Hata hivyo, waliiahidi Tume
kuongeza ushiriki wao mpana katika kusimamia na kuendeleza klabu hizo ndani ya vyuo vyao.
Kiasi cha wanafunzi wasiopungua 600 wakiwemo 400 kutoka Chuo Cha mafunzo ya Amali cha
Vitongoji na 200 kutoka chuo cha Daya, Mtambile kwa nyakati tofauti walihudhuria hafla hiyo
iliyowajenga kitaaluma na kuelezwa juu ya umuhimu wa kushiriki klabu kama hizo na umuhimu wake
wa kuanzishwa kwenye vyuo vyao.
MWISHO.