MAJALIWA AAGIZA USIMAMIAJI NA UDHIBITI WA UBORA WA ELIMU
▪️Asema lengo ni kuendelea kutoa wahitimu wenye uwezo wa kukidhi vigezo vya kimataifa ▪️Rais Dkt. Samia atoa milioni 100 kuchangia maendel...

WIZARA YA ARDHI YAWAJENGEA UWEZO WADAU WA MRADI WA UIMARISHAJI MIUNDOMBINU YA UPIMAJI
Written By CCMdijitali on Friday, January 31, 2025 | January 31, 2025
Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupitia Mradi wa Kuimarisha Miundombinu ya Upimaji na Ramani (LDI) imeendesha semina ya kuwajengea uwezo wadau wa mradi huo kutoka taasisi mbalimbali kuhusiana na namna mradi mradi huo unavyorahisisha kazi katika maeneo yao.
Semina hiyo imefanyika Januari 30, 2025 katika Kituo cha Ubunifu na Mafunzo ya Kijiografia kilichopo eneo la Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) jijini Dodoma ambayo imehusisha wataalamu kutoka taasisi mbalimbali za serikali zinazotegemea na kutumia taarifa za kijiografia kutekeleza majukumu yao.
Alizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhandisi Anthony Sanga, Mkurugenzi wa Upimaji na Ramani Bw. Hamdouny Mansoor amesema amesema semina hiyo inalenga kuwajengea uwelewa zaidi wataalamu hao kuhusu mradi wa LDI ili kuimarisha uhusiano mzuri uliopo miongoni mwa taasisi za Serikali hatua itakayosaidia kutekeleza mradi huo kwa pamoja kwa ufanisi zaidi.
Kutokana na umuhimu wa taasisi, tumeandaa semina hii ili kuwajengea uwelewa zaidi kuhusu mradi tukiamini hatua hii itaongeza uhusiano mzuri uliopo na taasisi na kwa pamoja kutekeleza mradi kwa ufanisi;. amesema Bw. Mansoir.
Kwa mujibu wa Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi,Mkurugenzi huyo wa Upimaji na Ramani ameongeza kuwa mradi huo wa LDI unaboresha miundombinu ya upimaji inayoleta taarifa zote za ardhi katika ukamilishaji wake.
Amesema, lengo kubwa la mradi huo wenye thamani ya dola milioni 65 unafadhiliwa na serikali ya Jamhuri ya Korea Kusini utasaidia kuandaa ramani za msingi kwa nchi nzima pamoja na kuboresha teknolojia ya upimaji.
Mradi huu una umuhimu wa kipekee katika sekta nyingine zinazotegemea taarifa za kijiografia katika kutekeleza majukumu yake na mfano ni katika miradi mikubwa ya kimkakati ya ujenzi wa miundombinu, utunzaji mazingira, utalii na udhibiti wa maliasili pamoja na ulinzi wa usalama wa nchi; amesema Mansoor.
Mradi huo ni uwekezaji mkubwa unaofanywa na serikali ili kuboresha huduma upatikanaji huduma na taarifa sahihi za kijiografia kwa wakati zikiwemo ramani za msingi ambazo ni nyenzo muhimu katika utawala wa ardhi hususan kupanga, kupima na kumilikisha.
-----------mwisho-----------
MAKAMU WA PILI WA RAIS ZANZIBAR- AFANYA ZIARA YA KUTEMBELEA HOSPITALI
Written By CCMdijitali on Wednesday, January 29, 2025 | January 29, 2025
MAKAMU WA PILI WA RAIS ZANZIBAR- ZIARA YA KUTEMBELEA HOSPITALI NA KIWANJA CHA MPIRA- CHAKE CHAKE PEMBA
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kutoa huduma bora za Afya kwa hospitali zote za Unguja na Pemba kwa lengo la kuhakikisha Afya za wananchi zinazidi kuimarika siku hadi siku.
Ameyasema hayo alipofanya ziara ya kukagua na kujionea hali ya upatikanaji wa huduma katika Hospitali ya Wilaya ya Chake - Chake iliyopo Vitongoji Kisiwani Pemba.
Amesema ameridhishwa na utoaji wa huduma za matibabu kwa wagojwa wanaofika hospitalini hapo ikiwa ni pamoja na kufanyiwa vipimo vyote muhimu na kupatiwa dawa wanazohitaji bila ya usumbufu wowote.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amesema amefarijika kuona kuwa wagonjwa wanaolazwa katika hospitali hio wanapatiwa chakula kwa wakati na ratiba ya chakula hospitalini hapo imepangwa kwa utaratibu maalum unaoendana na mahitaji ya lishe bora kwa afya ya binaadamu na kuutaka Uongozi wa Wizara ya Afya kuhakikisha huduma ya chakula inapatikana kwa wagonjwa wote wanaolazwa katika hospitali zote za Zanzibar.
Mhe.Hemed amesema mpango wa Serikali ni kuzidi kuiboresha Sekta ya Afya kwa kuendelea kujenga hospitali mpya kila Wialya na Mkoa kwa lengo la kuwasogezea wananchi huduma zote muhimu ndani ya Kisiwa cha Pemba na kuwapunguzia gharama wananchi ya kufuata matibabu nje ya Zanzibar.
Amezitaka kampuni zilizopata nafasi ya kutoa huduma hospitalini hapo na hospitali nyengine ndani ya Zanzibar kufanya kazi kwa uaminifu na uweledi wa hali ya juu kwa kuhakikisha huduma zote stahiki zinapatikana kwa wakati bila ya usumbufu wa aina yoyote.
Kwa upande wake Afisa Mdhamini Wizara ya Afya Pemba Ndugu KAMIS BILALI ALI amesema Mpango mkakati wa Wizara ya Afya ni kutoa huduma bora kwa wagonjwa wanaofika kufuata huduma katika hospitali zote nchini.
Bilali amesema hospitali ya Wilaya ya Vitongoji imekuwa ikizalisha gesi tiba mitungi mia mbili (200) kwa siku na kusambazwa katika hospitali zote kisiwani Pemba jambo ambalo limesaidia kuondoa usumbufu wa upatikanaji wa gesi tiba kwa wagonjwa wanaohitaji huduma hio kisiwani Pemba.
Amesema kabla ya kufungwa kwa mtambo huo wa kuzalisha gesi tiba hospitali hapo Serikali ililazimika kuagiza huduma hio kutoka sehemu nyengine za Tanzania hali ambayo ilikuwa inahatarisha afya za wagojwa wanaohitaji kupatiwa huduma hio.
Nao wagonjwa wanaofika hospitalini hapo akiwemo Bi. ASHA JUMA ABDALLA na Bwana ABDILAHI JUMA RAJAB wameishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuwawekea mazingira mazuri ya upatikanaji wa huduma za afya Mijini na Vijijini.
Wamesema kuwa wahudumu na madaktari waliopo hospitalini hapo wanatoa huduma bora na dawa zinapatikana kwa wakati sambamba na kupata chakula kwa wakati kwa gonjwa wote wanaolazwa hospitalini hapo.
Wakati huo huo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ametembelea na kukagua maendeleo ya Ukarabati wa Uwanja wa Mpira wa Gombani kisiwani Pemba na kuridhishwa na hatua ya ujenzi huo uliofikia asilimia 75 % unatarajiwa kumalizika mapema mwezi Machi 2025.
Mhe, Hemed amewataka wakandarasi wa ujenzi wa uwanja huo kuhakikisha wanamalizika kazi ndani ya muda wa makubaliano kwa ubora na viwango vya juu ili kutoa fursa kwa wanamichezo wa kisiwani Pemba kukitumia kiwanja hicho kwa kuchezea ligi kuu ya Zanzibar na michezo mingine ya Kitaifa na Kimataifa.
Ukarabati wa Uwanja huo unatarajiwa kumalizika mwezi machi 2025 ambao utajumuisha viwanja vya nje vitano (5) vya michezo mbali mbali pamoja na sehemu ya kuegesha magari kwa wanamichezo wanaofika uwanjani hapo.
![]() |
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akikagua na kujionea hali ya upatikanaji wa huduma za Afya katika Hospitali ya Wilaya ya Chake – Chake Vitongoji Kisiwani Pemba. |
Imetolewa na kitengo cha Habari ( OMPR )
29 / 01 / 2025.
MBUNGE UMMY MWALIMU ASHIRIKI MKUTANO WA HADHARA WA MKOANI TANGA
MBUNGE UMMY MWALIMU ASHIRIKI MKUTANO WA HADHARA WA MKOA TANGA KUUNGA MKONO MAAMUZI YA MKUTANO MKUU CCM TAIFA KUMPITISHA DKT SAMIA KUWA MGOMBEA URAIS 2025
Asema kwa mambo makubwa ya maendeleo yaliyotekelezwa Tanga Mjini wanaunga Mkono Maamuzi ya Mkutano Mkuu kwa asilimia 100 na watampa Dkt Samia kura za kishindo Octoba 2025
Makundi ya wananchi wakiwemo Wavuvi, Mafundi Gereji, madereva, Wajane, Bodaboda, Wahudumu wa Afya nao wajitokeza kwa wingi kuunga mkono Dkt Samia kupitishwa kugombea.
Mbunge wa Jimbo la Tanga Mhe Ummy Mwalimu tarehe 28/1/2025 ameshiriki mkutano wa hadhara uliondaliwa na CCM mkoa wa Tanga chini ya Mwenyekiti wa CCM Mkoa na Mjumbe wa Kamati Kuu Ndugu Rajab Abdulrahaman uliofanyika katika viwanja vya Community Center Kata ya Makorora Jijini Tanga.
Akiongea katika mkutano huo Mhe Ummy alieleza kuwa akiwa ni mbunge wa kuchaguliwa na wananchi wa Tanga Mjini anayo mamlaka ya kuwakilisha maoni yao kuwa watu wa Tanga Mjini wanaunga mkono kwa asilimia 100 Maamuzi ya Mkutano Mkuu wa CCM Taifa wa kumpitisha Dkt Samia kuwa kuwa Mgombea Urais katika Uchaguzi Mkuu ujao wa 2025.
Mbunge Ummy alieleza kuwa sababu za wananchi wa Tanga Mjini kuuunga mkono uamuzi huu ni kutokana na kazi kubwa na nzuri za maendeleo zilizofanywa na Rais Samia katika Jimbo la Tanga Mjini katika minne na nusu ya uongozi wake.
Kazi za Dkt Samia Tanga Mjni zinaonekama katika Sekta za Elimu, Afya, maji, Umeme hasa maeneo ya vijijini, uboreshaji wa miundombinu ya barabara, mikopo kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu na kubwa zaidi ni Maboresho ya Bandari ya Tanga kwa kuongezwa kina na sasa meli kubwa zinatia nanga katika Bandari ya Tanga na hivyo kuleta fursa za kiuchumi, biashara na uwekezaji Tanga. Mhe Ummy amesema kwa hili la Maboresho ya Bandari ya Tanga tu; Rais Dkt Samia hana deni na wana Tanga Mjini.
Mhe Ummy alimuhakikishia Mwenyekiti wa CCM Mkoa na wananchi kuwa Viongozi na wanachama wa CCM Wilaya ya Tanga watafanya kampeni usiku na mchana, za nyumba kwa nyumba ili kuhakikisha Dkt Samia anapata kura za kumwaga ili aendelee kuwa Rais wetu kwa miaka mingine mitano.
Hata hivyo Mhe Ummy amewataka wakazi wa Tanga Mjini kujitokeza kushiriki kwenye zoezi la maboresho la daftari la kudumu la wapiga kura wakati zoezi hilo litakapoanza mwezi Februari 2025 ili waweze kuandikishwa na kuweza kumpigia kura Dkt Sania, Mbunge na Madiwani watakaosimamishwa na CCM.
Mkutano huo wa hadhara ulihudhuriwa na wajumbe wa kamati ya siasa mkoa wakiongozwa na Mwenyekit wa CCM Mkoa na Mjumbe wa Kamati Kuu Ustadh Rajabu Abdurahmani, Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe Balozi Dkt Matilda Burian, Wajumbe wa Kamati za Siasa za Wilaya za Mkoa wa Tanga wakiongozwa na Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Tanga Meja Hamisi Bakari Mkoba, Viongozi wa Chama na serikali kutoka Wilaya mbalimbali za Mkoa wa Tanga sambamba na makundi ya wananchi wakiwemo Wavuvi, Mafundi Gereji, madereva, Wajane, Bodaboda, Wahudumu wa Afya.
MAKAMU WA PILI WA RAIS ZANZIBAR- AKABIDHI VIFAA VYA UJENZI KWA VIONGOZI WA UVCCM
Written By CCMdijitali on Sunday, January 26, 2025 | January 26, 2025
MAKAMU WA PILI WA RAIS ZANZIBAR- AKABIDHI VIFAA VYA UJENZI KWA VIONGOZI WA UVCCM- TUNGUU - MKOA WA KUSINI -UNGUJA
Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Ndugu Hemed Suleiman Abdulla amewataka Viongozi wa CCM, wanachama na wapenda maendeleo kujitolea katika kuchangia na kuunga mkono ujenzi wa miradi mbali mbali ya maendeleo inayojengwa na chama pamoja na Serikali kwa maslahi ya Taifa.
Ameyasema hayo wakati alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa chuo cha Umoja wa Vijana wa chama cha Mapinduzi ( UVCCM ) kinachojengwa Tunguu Mkoa wa Kusini Unguja na kuchangia vifaa mbali mbali ili kuendeleza ujenzi huo.
Mjumbe huyo wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa ambae pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amekabidhi saruji mifuko elf moja(1000), gari kumi (10) za mchanga na shilingi milioni tano (5) zitakazosaidia katika kuwapatia huduma vijana na CCM wanaojitolea katika ujenzi wa chuo hicho na kazi nyengine za Jumuiya ya UVCCM.
Mjumbe huyo wa kamati kuu ya halmashauri kuu amesema Chama cha Mapinduzi na Serikali kwa ujumla wanatambua kuwa nguvu na mchango wa vijana wa UVCCM katika kukijenga na kukiimarisha Chama hasa katika kusimamia ujenzi wa chuo cha UVCCM kitakachowafaundisha vijana kuwa watiifu na wazalendo kwa Taifa lao pamoja na kuwafundisha namna ya kujitegemea kiuchumi.
Mhe. Hemed amesema kuwa changamoto zinazowakabili UVCCM hasa katika ujenzi wa chuo hicho Serikali itazifanyia kazi ili kuweza kufanikisha malengo ya ujenzi huo kwa maslahi ya chama cha mapinduzi na kuiwezesha jumuiya ya Umoja wa vijana kupiga hatua kimaendeleo.
Aidha Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amesemea kuwa amefarajika kuona kazi kubwa inayofanywa na vijana wa umoja wa vijana wa CCM ya kujitolea katika kukiendelezaa na kukijenga chama ambapo ameahidi kuwa chama kitakuwaa bega kwa bega na vijana hao.
Sambamba na hayo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amewataka vijana kuendelea kuitunza amani iliyopo nchini hasa katika kupindi hiki cha kuelekea uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 na kuwaahidi kuwa watahakikisha chuo hicho kinamalizika katika viwango, ubora na hadhi ya hali ya juu kwa maslahi mapana ya Vijana wa CCM na Taifa kwa ujumla.
Nae Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) Mohamed Ali Mohamed ( KAWAIDA ) amesema dhamira ya ujenzi wa Chuo hicho ni kuendelea kutengeneza makada wa CCM na viongozi wenye uchungu na uzalendo wa nchi yao pamoja na kuwafunza namna bora ya kujiendeleza kiuchumia katika harakati zao za maisha.
Kawaida amemshukuru Mhe.Hemedi kwa maamuzi yake ya kutembelea ujenzi wa chuo hicho pamoja na mchango wake alioutoa katika kuendeleza ujenzi huo na kuahidi kuwa atahakikisha vijana wa CCM wanakuwa wamoja, watiifu na wenye utayari wa kukipambani chama ili kizidi kutekeleza Ilani kwa vitendo.
Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa UVCCM anaefanyia kazi zake Zanzibar Ndugu ABDI MAHMOUD ABDI amesema kumalizika kwa ujenzi wa chuo cha UVCCM utawanufaisha zaidi ya vijana elfu 4 ambao watapatiwa mafunzo mbali mbali chuoni hapo yakiwemo ya uzalendo kwa chama na Taifa lao pamoja stadi za maisha.
Amesema ujenzi huo utajumuisha mabweni mawili ya wanawake na wanaume, kumbi za mikutani, chumba cha wageni mashuhuri, Madarasa, zahanati pamoja na viwanja vya michezo mbali mbali ambapo mkandarasi na wajenzi wa chuo hicho ni vijana kutoka UVCCM.
Abdi amesema UVCCM wanaishukuru Serikali kwa kuendelea kuwapa kipaombele vijana na kuomba kusaidiwa kutatuliwa changamoto zao zinazowakabili ikiweno ya kuvamiwa kwa eneo lao lililopa Tunguu ambalo limetengwa maalum kwa ajili ya shuhuli za UVCCM.
Imetolewa na Kitengo cha Habari ( OMPR )
Leo tarehe..26 / 01 / 2025
JK AIPA PPAA CHANGAMOTO KUOKOA FEDHA ZA SERIKALI KATIKA MIRADI
Written By CCMdijitali on Saturday, January 25, 2025 | January 25, 2025
Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Kikwete ameipa Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) changamoto ya kuangalia jinsi ununuzi wa umma unavyoweza kuokoa fedha za umma na kuhakikisha kuwa Serekali inapata thamani ya fedha katika miradi yake inayoitekeleza.
Mheshimiwa Kikwete ametoa changamoto hiyo wakati alipotembelea banda la PPAA katika maonesho ya Wiki ya Sheria yaliyoanza tarehe 25 Januari, 2025 katika viwanja vya Nyerere Square Jijini Dodoma.
“Wakati nilipokuwa Rais kuna halmashauri moja ilijenga jengo lake kwa kutumia shilingi milioni 15 kwa jitihada zao wenyewe, lakini wakaambiwa kwamba wasiendelee na utaratibu ule lazima zabuni itangazwe, baada ya zabuni kutangazwa wakanionesha nyumba iliyojengwa kwa milioni 45,” alisema Dkt. Kikwete.
Hivyo kuna umuhimu wa wadau wa sekta ya ununuzi wa umma kuhakikisha kuwa Sheria ya ununuzi wa umma inasaidia kupatika kwa thamani halisi ya fedha katika miradi mbalimbali.
Awali Afisa Mwandamizi wa PPAA, Bw. Stanley Jackson alimweleza Mhe. Dkt. Kikwete kuwa kwa kipindi cha takribani miaka minne, PPAA imeweza kushughulikia mashauri 162 yaliyotokana na michakato ya Ununuzi wa Umma ambapo katika mashauri hayo, PPAA ilizuia utoaji tuzo kwa zabuni 35 zenye thamani ya takribani bilioni 583.6 kwa wazabuni wasio na uwezo wa kifedha pamoja na wale waliokosa sifa za kitaalamu za kutekeleza zabuni husika.
“Hatua hiyo iliepusha utekelezaji usioridhisha wa miradi unaosababisha upotevu wa fedha za umma na kuchelewesha maendeleo stahiki kwa wananchi,” alisema Bw. Jackson.
Pamoja na mambo mengine, Bw. Jackson aliongeza kuwa Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) kwa kushirikiana na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) imekamilisha utengenezaji wa moduli ya kuwasilisha na kushughulikia rufaa na malalamiko kwa njia ya kielektroniki (Complaint and Appeal Management Module) katika Mfumo wa Kielektroniki wa Ununuzi wa Umma (NeST).
Bw. Jackson aliongeza kuwa, kukamilika kwa Moduli hiyo kutawawezesha wazabuni kuwasilisha kwa njia ya kielektroniki malalamiko na rufaa zitokanazo na michakato ya ununuzi wa umma kwa Taasisi Nunuzi na Mamlaka ya Rufani pasipo kulazimika kutembelea ofisi husika.
“Ili kuwawezesha wazabuni na watendaji wa taasisi nunuzi kutumia moduli hiyo, PPAA kwa kushirikiana na PPRA imeandaa mafunzo ya matumizi ya moduli ya kushughulikia malalamiko na rufaa kwa njia ya kielektroniki yatakayoambatana na tamko rasmi la kuanza kwa matumizi ya moduli hiyo.
…..Mafunzo haya yanawalenga wazabuni na watendaji wa taasisi nunuzi wa mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Kagera, Musoma, Geita na Simiyu. Mafunzo yatafanyika kuanzia tarehe 4 - 6 Februari, 2025 Jijini Mwanza katika Ukumbi wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) uliopo Capripoint,” alisema Bw. Jackson
Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) ni taasisi inayojitegemea chini ya Wizara ya Fedha iliyoundwa kwa mujibu wa Kifungu cha 112 cha Sheria ya Ununuzi wa Umma Namba 10 ya mwaka 2023. PPAA imepewa kisheria jukumu la kupokea na kusikiliza malalamiko na rufaa zinazotokana na michakato ya Ununuzi wa Umma na kufungiwa kwa wazabuni (blacklisting of tenderers) kushiriki katika michakato ya Ununuzi wa Umma na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA).
Maadhimisho ya wiki ya sheria yameongozwa na Kauli Mbiu: “Tanzania ya 2050: Nafasi ya Taasisi zinazosimamia Haki Madai katika kufikia Malengo Makuu ya Dira ya Taifa ya Maendeleo”.
MAKAMU WA PILI WA RAIS ZANZIBAR- AZINDUA MASHINDANO YA QUR-AN- AFRIKA- MADINATULBAHARI MBWENI
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Alhajj Hemed Suleiman Abdulla amesema hatua ya kuwashirikisha watoto katika harakati mbali mbali za dini ya kiislamu ikiwemo mashindano ya kuhifadhi Qur-an ni njia sahihi inayochangia kuwakuza watoto kimaadili na kiroho pamoja na tabia njema.
Ameyasema hayo katika uzinduzi wa Mashindano ya Kuhifadhi Qur-an Afrika uliyofanyika katika Ukumbi wa Hotel ya Madinat Al Bahr Mbweni jijini Zanzibar.
Alhajj Hemed amesema kuwa mashindano ya Kuhifadhi Qur-an yanawajenga watoto kuwa na tabia njema zenye kumtii Mwenyezi Mungu na kuifahamu vyema dini yao sambamba na kuwaepusha kujiingiza katika vitendo viovu ukiwemo Wizi, Ujambazi, Ubakaji na Matumizi ya madawa ya kulevya.
Amesema jamii inapaswa kufahamu kuwa jukumu la kuhimiza na kusimamia maadili mema ni wajibu wa kila mmoja na kwa nafasi yake kuhakikisha suala la maadili linapewa kipaombele ili vijana waweze kuishi katika miongozo mema ya dini ya kiislamu na kuepuka kufuata mila, silka na desturi za kigeni zinazokwenda kinyume na maamrisho Allah ( S.W )
Alhajj Hemed amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inatambua na kuthamini mchango mkubwa unaotolewa na Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC) kwa kushirikiana na Afisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar katika kuijenga jamii yenye maadili mema na kuahidi Serikali itaendelea kuunga Mkono juhudi hizo kwa kutoa kila aina ya ushirikiano utakaohitajika ili kuendeleza dini ya Kiislam na kuimarisha maadili mema nchini.
Sambamba na hayo Mhe. Hemed amesema Zanzibar imeweza kupiga hatua kubwa ya kimaendeleo katika sekta mbali mbali kutokana na kuwepo kwa amani na mshikamano hivyo ametoa wito kwa wananchi kuzidi kuitunza amani na umoja uliopo nchini pamoja na kuwataka Mashekhe, maimamu, wahadhiri, viongozi wa dini na viongozi wa vyama vya kisiasa kuwataka wafuasi wao kudumisha amani na mshikamano hasa katika kupindi hiki cha kuelekea uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC) ambao ndio waandaaji wa Mashindano hayo Bwana RAMADHAN ATHUMANI BUKINI amesema lengo la kamati ya Mashindano ya kuhifadhi Qur-an ni kuona mashindano hayo yanakuwa makubwa na kushirikisha nchi zote duniani kwa na lengo la kuwaandaa vijana kiroho na kiimani katika kuiisimamisha dini ya kiislamu.
Bukini amesema mashindano hayo ya kuhifadhi Qur-an Afrika yanayotarajiwa kufanyika mwezi Machi 2025 na kushirikisha nchi tisa(9) ikiwemo Afrika Kusini, Nigeria, Senegal, Komoro, Kenya, Algeria, Kongo, Tanzania Bara na Wenyeji Zanzibar yatasaidia kuwaendeleza vijana katika kukihifadhi na kukisoma kwa weledi kitabu kitakatifu cha Qur-an .
Amesema hamasa ya Mashindano hayo imekuwa ni kubwa jambo ambalo limepelekea nchi mbali mbali duniani kuwa na utayari wa kushiriki katika mashindano hayo na kuahidi kila mwaka kuongeza idadi ya nchi washiriki pale ambapo hali ya udhamini itaimarika zaidi.
Akitoa salamu za Afisi ya Mufti Mkuu Zanzibar katika uzinduzi wa Mashindano hayo Katibu Mtendaji Ofisi ya Mufti Mkuu Zanzibar Sheikh Khalid Ali Mfaume amewataka waislamu kuekeza katika mambo ya kheri na kuwa tayari kujitoa kwa Elimu zao, Mali zao pamoja na nguvu zao katika kuilingania na kuisimamisha dini ya Kiislamu.
Sheikh Mfaume amesema ni wajibu wa Kila muislamu kwa nafasi yake kuunga mkono mashindano hayo kwa kuyatangaza ili yaweze kutambulika ulimwenguni kote na waislamu kupata fursa ya kushiriki kwa wingi katika mashindano hayo.
Imetolewa na Kitengo cha Habari ( OMPR )
Leo tarehe…25 / 01 / 2025.
SERIKALI YAZISHAURI TAASISI KUJIORODHESHA KWENYE SOKO LA HISA LA DAR ES SALAAM - DSE
Written By CCMdijitali on Friday, January 24, 2025 | January 24, 2025
Serikali imezishauri taasisi mbalimbali nchini kujiorodhesha kwenye Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) ili kutoa fursa kwa wananchi kushiriki kukuza uchumi wao binafsi na uchumi wa nchi kwa njia za kidijitali.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), wakati wa hafla ya kuorodhoreshwa rasmi kwa Hati Fungani ya Benki ya Azania ijulikanayo kama Bondi Yangu, katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), hafla iliyofanyika katika Ofisi za DSE, jijini Dar es Salaam.
Mhe. Dkt. Nchemba alisema kuwa Uorodheshwaji wa Hatifungani hiyo utakuza ukwasi kwa wawekezaji kwa kutoa mwanya wa kuuza na kununua kupitia soko hilo na utaleta chachu kubwa katika kukuza Soko la Hisa la Dar es Salaam ambalo limekuwa mstari wa mbele katika kutoa fursa kwa watanzania kushiriki katika sekta rasmi ya fedha.
“Taarifa mbalimbali zilizotolewa zinaonesha mauzo ya Bondi Yangu yamekuwa ya mafanikio makubwa kwa kukusanya jumla ya Shilingi bilioni 63.3 ambayo ni mafanikio ya asilimia 210.9, mafanikio ya namna hii ni nadra kwa mtoaji wa kwanza wa Hatifungani na hii inadhihirisha kuwa Benki ya Azania imeanza na mwanzo mzuri wa utoaji wa Hatifungani yake na malengo yao ni kukusanya zaidi ya TZS 100 bilioni ili kusaidia makundi ya wanawake, vijana na wajasiriamali wadogo kuweza kushirikishwa katika sekta rasmi ya fedha hapa nchini” alisema Dkt. Nchemba.
Dkt. Nchemba aliongeza kuwa Serikali itaendelea kuhakikisha kuboresha mazingira ya kufanya biashara ili taasisi mbalimbali ziendelee kuja na ubunifu wenye tija ili kusaidia utoaji wa mikopo nafuu kwa makundi mbalimbali ya kinamama, vijana na wajasiriamali na kuleta chachu zaidi katika kuwawezesha wale ambao wanakwama kupata huduma rasmi za kibenki kuwezeshwa kiuchumi.
Aidha, Dkt. Nchemba alitoa wito kwa wananchi na wawekezaji kuchangamkia fursa ya awamu ya pili ya Hatifungani pale itakapozinduliwa rasmi ili kuongeza chachu ya maendeleo kwa taifa letu.
“Napenda kuwahakikishia wawekezaji na wananchi kwa ujumla kuwa Serikali yetu chini ya Uongozi mahiri wa Mama yetu, Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itaendelea kuweka mazingira bora ya uwekezaji katika sekta ya fedha na hasa kwenye masoko ya mitaji na dhamana” aliongeza Dkt. Nchemba.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Azania, Dkt. Esther Mang’enya, alisema kuwa hadi sasa jumla ya wawekezaji 650 wamefungua akaunti za CDS kuwawezesha kushiriki katika mauzo ya Bondi Yangu na shughuli zingine za masoko ya mitaji na dhamana ambapo zaidi ya asilimia 97.3 ya wawekezaji walioshiriki katika “Bondi Yangu” ni wawekezaji mmoja mmoja (retail investors).
Aidha, Afisa Mtendaji Mkuu wa Soko la Hisa la Dar es Salaam, Bw. Peter Nalitolela, alisema kuwa thamani ya uwekezaji wa hatifungani katika soko hilo imeendelea kuongezeka na sasa imefikia takribani shilingi trilioni 27.6, huku idadi ya wawekezaji ikiwa imefikia 637,137.
Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), CPA Nicodemus Mkama, amepongeza mafanikio hayo, akibainisha kuwa yanatokana na mazingira wezeshi ya uwekezaji yaliyowekwa, ikiwa ni pamoja na kuondolewa kwa kodi ya zuio kwenye faida ya hatifungani za taasisi.